Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kumbukizi ya mauaji ya kimbari Rwanda, Mkuu wa MONUSCO ataka stahamala

Kumbukizi ya mauaji ya kimbari Rwanda, Mkuu wa MONUSCO ataka stahamala

Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC, Martin Kobler, amesema wakati Rwanda na dunia wakikumbuka mateso ya mauaji ya kimbari yaliyofanyika miaka 21 iliyopita, ni vema kukumbuka umuhimu wa kujenga amani kwa pamoja.

Katika ujumbe wake uliotolewa na Ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini humo, MONUSCO kupitia mtandao wa kijamii wa Twitter,Bwana  Kobler amenukuliwa akisema dunia ikipanda mbegu ya amani leo , itazuia vita na mauaji ya kesho, akisema jamii ya kimataifa inapaswa  kujenga pamoja dunia yenye amani kwa ajili ya vizazi vijavyo.

Ili kuepusha mauaji mengine ya kimbari nchini Rwanda,  Baraza la Usalama kupitia azimio lake nambari 2211 la tarehe 26, Machi, 2015, limekariri umuhimu wa kuondoa tishio la kundi la waasi la FDLR mashariki mwa DRC, likieleza kwamba miongoni mwa waasi hao ni watekelezaji wa mauaji ya kimbari ya Rwanda, wengine wakiendelea kuua watu kwa misingi ya kikabila katika maeneo hayo.