Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

UN Women kwenye ziara ya mshikamano na Sierra Leone

UN Women kwenye ziara ya mshikamano na Sierra Leone

Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika linalohusika na masuala ya wanawake, UN Women,  Phumzile Mlambo-Ngcuka, yumo ziarani nchini Siera Leone, akidhamiria kuonyesha mshikamano wa shirika hilo na serikali na watu wa Sierra Leone, wakati huu ambapo taifa hilo linaendelea kukabiliana na athari za mlipuko wa Ebola nchini humo, ambao uliwaambukiza zaidi ya watu 10,000, kuwaua 3480 na kuacha zaidi ya mayatima 3,000.

Afisa huyo wa ngazi ya juu wa Umoja wa Mataifa anatazamiwa kukutana na Rais Ernest Bai Koroma, maafisa wengine wa serikali na wadau ili kujadili kuhusu masuala ya jinsia yanayohusiana na mlipuko wa kirusi cha Ebola.

Ujumbe wa Bi Mlambo-Ngcuka umakariri uungaji mkono wa Umoja wa Mataifa kwa ajenda ya maendeleo ya taifa hilo na mkakati wake wa tatu wa kupunguza umaskini na kuongeza utajiri.

Miongoni mwa  mambo aliyopanga kushiriki akiwa Sierra Leone ni kuzinduliwa kwa mradi wa afya ya uzazi katika hospitali ya serikali ya Kenema, ambao umefadhiliwa na UN Women.