Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mustakhbali wa mpango wa nyuklia Iran watoa matumaini

Mustakhbali wa mpango wa nyuklia Iran watoa matumaini

Makubaliano yamefikiwa mjini Vienna, Austria kuhusu mustakhbali wa masuala ambayo hayapatiwi suluhu juu ya mpango wa nyuklia wa Iran.

Hiyo ni kwa mujibu wa shirika la kimataifa la nishati ya atomiki, IAEA na inafuatia mazungumzo kati ya Mkurugenzi Mkuu Yukiya Amano na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran S. Abbas Araghchi mjini humo.

Taarifa ya IAEA inasema mazungumzo hayo yalikuwa muhimu na kuimarisha maelewano kati ya pande mbili hizo ambapo shirika hilo limeongeza muda wake wa ufuatiliaji na uthibitishaji wa mpango wa nyuklia wa Iran hadi mwezi Juni mwaka huu.

Wawili hao wametambua umuhimu wa kuendeleza mazungumzo ambapo mapema mwezi huu Bwana Amano alikuwa na mazungumzo na waziri wa mambo ya nje wa Iran Mohammad Javad Zarif mjini Munich.

Maafisa wa Iran mara kwa mara wamekuwa wakisisitiza kuwa mpango wa nyuklia wa nchi hiyo ni kwa matumizi salama hata hivyo IAEA haijasema lolote kuhusu kauli hiyo.

Mwaka 2003, dunia ilibaini kuwa Iran imekuwa ikificha shughuli zake za n yuklia kwa miaka 18 ikiwa ni kinyume na wajibu wake wa mkataba wa kimataifa wa kutotumia nyuklia.