Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Uislamu wenye msimamo mkali ndio tishio kubwa zaidi kwa amani duniani- Israel

Uislamu wenye msimamo mkali ndio tishio kubwa zaidi kwa amani duniani- Israel

Mwakilishi wa Kudumu wa Israel kwenye Umoja wa Mataifa, Balozi Ron Prosor, amesema leo kwamba iwapo dunia inataka kuzuia mauaji ya halaiki kama yale ya Holocaust yasitokee tena, ni lazima isadiki na kung’amua kuwa Uislamu wenye msimamo mkali ndio tishio kubwa zaidi kwa amani na usalama duniani. Balozi Prosor amesema hayo leo, wakati wa hafla maalum ya kuadhimisha miaka 70 tangu kukombolewa kwa kambi ya Auschwitz-Birkenau, iliyotumiwa na serikali ya Nazi, Ujerumani, kutekeleza mauaji ya halaiki.

 “Tuna wajibu wa kuchukua hatua. Ni lazima tuwe waangalifu, kutambua ishara za onyo. Ni lazima tulaani wote wanaoongozwa na ubaguzi. Ni lazima tuelimishe kizazi kijacho kuvumiliana na kuelewana, kwani ni kupitia katika elimu tu, ndipo mabadiliko yanawezekana.”

Kwenye hafla hiyo iliyoandaliwa na Ubalozi wa Poland kwenye Umoja wa Mataifa, Balozi Prosor ametoa wito uwepo ushirikiano katika kuhakikisha maadili ya uanadamu yanalindwa na uovu kushindwa.

“Pamoja, ni lazima tusimame kwa ujasiri na kujitoa, kulinda uhuru wetu, maadili yetu, na kupambana na wale wanaotaka kuvitwaa hivi. Ni hapo tu ndipo tutaweza kusema, kamwe isitokee tena, na kujua kuwa maneno hayo yana maana.”