Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Sudan Kusini inakaribia kutumbukia kwenye hali mbaya-FAO

Sudan Kusini inakaribia kutumbukia kwenye hali mbaya-FAO

Ripoti mpya zinaonyesha kwamba mamia ya wananchi huko Sudan Kusin wameyakimbia makazi yao na kusababisha mifugo waliyokuwa wakimiliki kuingia mtawanyikoni jambo ambalo linazusha wasiwasi wa kuzuka kwa magonjwa ya mlipuko na hivyo kuvuruga ustawi wa maisha ya wakulima na wafugaji.

Uchunguzi uliofanywa na maofisa wa Shirika la Chakula na Kilimo Duniani FAO ambao hivi karibuni walizuru eneo hilo unaonyesha kuwa mifugo mingi imekuwa ikiranda randa ovyo kutokana na wamiliki wake kukimbia mapigano.

Hali hiyo imezusha wasiwasi mkubwa miongoni mwa jamii ya wakulima na wafugaji huku wasiwasi pia ukiongezeka miongoni mwa wafugaji wenyewe.

Kwa hivi sasa FAO pamoja na washirika wake wameanzisha jitihada za kukabiliana na uwezekano wa kuzuka kwa magonjwa ya mlipuko katika eneo hilo. Maofisa hao FAO wamezitembelea jamii za wafugaji na wakulima kwa ajili ya kutathmini hatua zinazopaswa kuchukuliwa kabla ya hali haijakuwa mbaya.