Ban akiwa Sierra Leone azungumzia mshikamano dhidi ya Ebola
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon anaendelea na ziara yake ya mataifa yaliyoathiriwa zaidi na janga la Ebola huko Afrika Magahribi, ambapo leo ametembela Sierra Leone.
Akizungumza katika kituo cha Hastings, cha kutibu Ebola, Bwana Ban amesema kipindi cha miezi kadhaa baada ya Ebola kimeghubikwa na majonzi kwani kirusi hicho kimebadilisha siyo tu maisha ya watu bali tamaduni zao ikiwemo zile za mazishi.
Katibu Mkuu amesema Ebola imewaacha mamia na maelfu ya watu wakiwa na njaa huku watoto wakibakia yatima, mamilioni hawaendi shule huku huduma muhimu za afya kwa watoto zikitumbukia.
Hata hivyo Ban ameelezea mshikamano wa Umoja wa Mataifa na watu wa Sierra Leone, akisema Ebola ni janga la dunia nzima hivyo ni muhimu kuudhibiti kule ulikojikita na hatimaye kufikia lengo la kutokuwa kabisa na mgonjwa.