UNOWA yalaani mashambulio mapya Nigeria
Mwakilishi maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa huko Afrika Magharibi, UNOWA, Mohamed Ibn Chambas ameshutumu vikali kurejea mpya kwa wimbi la mashambulio dhidi ya raia wasio na hatia Kaskazini-Mashariki mwa Nigeria.
Taarifa ya UNOWA imemkariri Chambas akisema vitendo hivyo ikiwemo kutekwa nyara kwa wanawake na watoto vinazidi kuongezeka na ametoa wito kwa serikali ya Nigeria kudhibiti matukio hayo na wahusika wafikishwe mbele ya sheria.
Chambas ambaye pia ni mwakilishi wa ngazi ya juu wa Katibu Mkuu huko Nigeria amekumbusha kuwa Umoja wa Mataifa uko na familia za wahanga wa matukio hayo ya mashambulizi, wananchi na serikali ya Nigeria.