Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Uamuzi kutoka COP20, umefungua njia kwa mkataba 2015:Ban

Katibu Mkuu wa UM alipohutubia COP20 wakati wa ufunguzi. (Picha:UN/Mark Garten)

Uamuzi kutoka COP20, umefungua njia kwa mkataba 2015:Ban

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-Moon amesema uamuzi uliofikiwa huko Lima, Peru mwishoni mwa mkutano wa 20 wa mabadiliko ya tabianchi, COP20, unafungua njia ya kufikiwa kwa mkataba wa kimataifa wa masuala hayo hapo mwakani.

Taarifa ya msemaji wa Umoja wa Mataifa iliyotolewa baada ya kumalizika kwa mkutano huo wa wiki mbili, imemkariri Ban akikaribisha matokeo yake ikiwemo kupitishwa kwa nyaraka iitwayo Wito wa Lima kwa hatua kuhusu tabianchi.

Katibu Mkuu amesema washiriki kutoka pande 196 wanachama wa mfumo wa mkataba wa mkataba wa kimataifa kuhusu mabadiliko ya tabianchi, UNFCCC wametoa ahadi muhimu za kutekeleza ikiwemo hatua watakazochukua kupungua utoaji wa hewa chafuzi na kuzuia vitendo vya kibinadamu vinavyoathiri sayari ya dunia.

Kwa mantiki hiyo ametaka pande zote katika mkutano wao wa kwanza mwezi Februari mwakani ziwe na mashauriaon ya kina juu ya rasimu ya mkataba wa mwaka 2015 kutokana na kikao cha Lima.

Wakati wa mkutano wa Lima, ahadi kwa ajili ya mfuko wa miradi rafiki ya mazingira zilivuka lengo la dola Bilioni 10 lililokuwa limewekwa awali.