Cristina Gallach kuongoza idara ya mawasiliano ya umma ya UM
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon amemteua Cristina Gallach wa Hispania kuwa msaidizi wake kwa masuala ya habari na mawasiliano kwa umma.
Bi. Gallach anachukua nafasi iliyoachwa na Peter Launsky-Tieffenthal wa Austria aliyemaliza muda wake ambapo Ban amemshukuru kwa mchango wake wakati akiongoza idara hiyo.
Taarifa ya msemaji wa Umoja wa Mataifa imesema Bi. Gallach ambaye ataongoza idara ya habari na mawasiliano ya umma ya umoja huo ana uzoefu katika tasnia ya mawasiliano, diplomasia, uongozi, masuala ya kimataifa na menejimenti.
Halikadhalika amewahi kuwa mwandishi wa habari wa magazeti, redio na televisheni.
Hadi anapata uteuzi huu, Bi. Gallach amekuwa anaongoza idara ya uhusiano wa umma ya Baraza la Muungano wa Ulaya.