Vurugu Burkina Faso, Ban aeleza wasiwasi, atuma mjumbe wake
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon amesema anafuatilia kwa wasiwasi mkubwa kuendelea kuzorota kwa hali ya usalama nchini Burkina Faso kutokana na matukio ya hivi karibuni.
Taarifa ya msemaji wa Umoja huo imemkariri Ban akitoa wito kwa pande zote nchini humo kuacha kutumia ghasia na badala yake kuwa watulivu na kutumia mashauriano kusuluhisho mambo yote yanayoleta tofauti kati yao.
Katibu mkuu ameelezea masikitiko yake kutokana na vifo vilivyosababishwa na matukio ya hivi karibuni.
Tayari amemwagiza mwakilishi wake maalum kwa Afrika Magharibi Mohammed Ibn Chambas kufanya ziara huko Burkina Faso siku ya Ijumaa akisema ziara hiyo itafanyika kwa pamoja na Muungano wa Afrika na Jumuiya ya nchi za Afrika Magharibi, ECOWAS.