Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Akiwa Cairo, Ban azungumzia msingi bora wa kuijenga upya Gaza

Ban akiwa Cairo kwenye kongamano kuhusu kuikarabati Gaza. Picha @ UM

Akiwa Cairo, Ban azungumzia msingi bora wa kuijenga upya Gaza

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon, amesema kuwa Gaza haiwezi kujengwa tena kwa msingi hafifu wa kisiasa, wakati akizungumza mjini Cairo kwenye kongamano la kuikarabati Gaza. Bwana Ban ambaye yuko ziarani Mashariki ya Kati, amesema kuwa jamii ya kimataifa inatambua dhahiri mahitaji makubwa ya Gaza, na hivyo imeonyesha utashi wake wa kuchukua hatua mathubuti.

Katibu Mkuu amesema, kwa kutambua kuwa Gaza haiwezi kujengwa kwa msingi hafifu kisiasa, Umoja wa Mataifa utaendelea kuunga mkono serikali ya maafikiano ya kitaifa.

Bwana Ban amesema pia kuwa kongamano hilo la kuikarabati Gaza linapaswa liwe ndilo la mwisho la aina yake, akiongeza kuwa mzunguko wa kukarabati na kubomoa ni lazima ukomeshwe.

Katibu Mkuu amesema wafadhili wamechoshwa, lakini pia madhara kwa watu wa Gaza na umwagaji damu vimezidi, na hivyo basi sasa ndio wakati wa kubuni barabara mwafaka ya amani kati ya Waisraeli na Wapalestina.