Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kila siku watoto 39,000 wanafungishwa ndoa za lazima: UN-Women

Watoto wa kike wakiwa darasani. (Picha-UN-Women-tovuti)

Kila siku watoto 39,000 wanafungishwa ndoa za lazima: UN-Women

Leo ni siku ya mtoto wa kike duniani ambapo maudhui ni kumlinda na kumwezesha mtoto wa kike barubaru ambao ni kundi lenye umri wa kati ya miaka 11 hadi 19.

Mkurugenzi Mtendaji wa shirika la Umoja wa mataifa linaloshughulikia masuala ya wanawake, Phumzile Mlambo-Ngucka amesema kundihilolinakumbwa na madhila kadhaa ikiwemo ndoa za umri mdogo na baadhiyaokukumbwa na ukatili tena na watu walio karibu nao.

Amesema kila siku wasichana Elfu 39 wanaozeshwa kabla ya kufikia umri wa miaka 18 na kwamba iwapo mwelekeo huo utaendelea ifikapo mwaka 2020 kutakuwepo na watoto wa wakike Milioni 140 walioozwa.

Kwa mantiki hiyo Mkuu huyo wa UN-Women amesema ujumbe wa mwaka huu umekuja wakati muafaka ili kukomboa kundi hilo.

(sauti ya Phumzile)

 “Suala la kulinda wasichana dhidi ya ukatili wa aina yoyote na kuendeleza uwezeshaji wao limo katika ajenda ya dunia, kwa sababu tunaamini kuwa wasichana wanafahamu wanachotaka, wana dira na wana uwezo, na wao ni viongozi wetu na tunawafuatilia.”

Umoja wa Mataifa unasema ingawa nchi nyingi zinafikia lengo la kuweka uwiano wa mtoto wa kike na wa kiume katika uandikishaji shule ya msingi,  bado wasichana wengi wanakosa stadi za kusoma na kuandika.

Halikadhalika Umoja wa Mataifa umesema pamoja na kikwazo hicho cha elimu bado kuna mila na desturi zinazofanya wasichana wakose haki zao za msingi.