Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Misaada ya UNICEF na WFP yafikia zaidi ya watu 500,000 Sudan Kusini

Nchini Sudan Kusini WFP na UNICEF kwa pamoja wanatoa msaada wa chakula kwa watoto wanao ugua na utapiamlo.Picha ya WFP/fb

Misaada ya UNICEF na WFP yafikia zaidi ya watu 500,000 Sudan Kusini

Mpango wa pamoja wa 25 wa mashirika mawili ya Umoja wa Mataifa lile la watoto, UNICEF na la mpango wa chakula, WFP wa kupeleka chakula kwenye maeneo magumu zaidi kufikika huko Sudan Kusini umenufaisha watu zaidi la 500,000.

Maeneo hayo ni yale yaliyokumbwa na mapigano na yako ndani zaidi ambapo misaada ilifikishwa kwa ndege na helikopyta kwenye jimbo la Jonglei. Misaada hiyo ni pamoja na chakula chenye virutubishi, chanjo kwa watoto kama ile ya Surua na Polio pamoja na vifaa vya kujisafi.

Takwimu zinaonyesha kuwa kati ya idadi hiyo, kuna watoto 100,000 walio na umri wa chini ya miaka mitano ambao walinufaika pia na chanjo.

James Elder ni mtaalamu mkuu wa mawasilino kutoka UNICEF.

(Sauti ya James)

“Idadi ya watu wasio na uhakika wa chakula Sudan Kusini kwa kuzingatia takwimu za wiki iliyopita ni Milioni 1.9. Na pia kuna idadi nyingine ya 200,000 ambayo ni ya watoto walio na umri wa chini ya miaka mitano, ambao wanaweza kukabiliwa na utapiamlo uliokithiri hofu yetu ni watoto 50,000 wanaoweza kufariki dunia iwapo hawatapatiwa msaada zaidi.”

Mpango huo wa pamoja wa UNICEF na WFP ulijumuisha wataalamu wa chakula na lishe, huduma za kujisafi na elimu.