Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Usalama nchini Libya bado ni kitendawili:UNSMIL

Bernadino Leon, Mkuu wa Ujumbe wa Mataifa nchini Libya UNSMIL, alipozungumza na waandishi wa Habari, mjini Tobruk, ambapo Bunge la Libya limelazimika kuhamia. Picha ya UNSMIL.

Usalama nchini Libya bado ni kitendawili:UNSMIL

Mwakilishi huyo amesema, ujumbe wa Umoja wa Mataifa UNSMIL ukitimiza miaka mitatu nchini Libya, hali inaendelea kuzorota, na makombora yanayorushwa katika maeneo ya mji mkuu Tripoli yamelazimisha maelfu ya watu kukimbia makazi yao.

Kwa upande wa kisiasa, ameeleza kwamba mamlaka za serikali zimedhoofika sana, wakati bunge lililazimika kuhamia mashariki mwa nchi, akiziomba pande zote za kisaisa kuwajibika na kusisitiza umuhimu kwa uongozi jumuishi.

(Sauti ya Bernadino)

"Juhudi zinazolenga kutatua mzozo na kuanzisha tena utaratibu wa kisiasa haziwezi kufanikiwa katika hali ya mapigano. Narudia kuziomba pande husika kuhusu haja ya kusikia ombi la Baraza la Usalama kusitisha mapigano nchini humo" 

Kwa upande wake, Naibu Mwakilishi wa Kudumu wa Rwanda kwenye Umoja wa Mataifa Olivier Nduhungirehe ametoa maelezo kuhusu vikwazo vilivyowekwa dhidi ya Libya.

(Sauti ya Olivier)

"Jopo limebaini kuzorota haraka kwa hali ya usalama nchini Libya, pamoja na kushindwa kufuatilia uwakala wa vifaa vya kijeshi na kushindwa kabisa kudhibiti usafiri za meli na za ndege na mamlaka za Libya, vyote vikiashiria kwamba idadi kubwa ya vifaa vya kijeshi imewafikia wanamgambo"