Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kazi ya kukagua kura Afghanistan yakamilika:UM

Ukaguzi na uhakiki wa kura kufuatia awamu ya pili ya uchaguzi wa Rais nchini Afghanistan. (Picha@Fardin Waezi / UNAMA)

Kazi ya kukagua kura Afghanistan yakamilika:UM

Kazi ya ukaguzi wa kura za awamu ya pili ya uchaguzi wa Rais uliofanyika nchini Afghanistan tarehe 14 mwezi Juni mwaka huu imekamilika.

Taarifa hizo ni kwa mujibu wa mshauri mwandamizi wa Umoja wa Mataifa kwenye tume ya huru ya uchaguzi nchini Afghanistani, Richard Chambers ambaye amesema hatua hiyo inakamilisha jukumu hilo adhimu lililopatiwa umoja huo.

Amesema walitekeleza jukumu kama walivyoagizwa na wagombea wawili wa nafasi hiyo Dkt. Ashraf Ghani na Dkt, Abdullah Abdullah.

Habari zinasema baada ya tangazo hilo, taasisi husika za uchaguzi nchini Afghanistan zitasikiliza malalamiko kutoka pande husika,ikifuatiwa na kuthibitisha matokeo na hatimaye kutangaza rasmi mshindi.

Umoja wa Mataifa umetoa shukrani zake kwa tume huru ya uchaguzi Afghanistan kwa ushirikiano wake pamoja na waangalizi wa kimataifa na wale wa kitaifa bila kusahau ofisi za kibalozi kwa mchango wao uliowezesha kufanyika kwa zoezi hilo kwa uwazi.