Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Maambukizi ya HIV miongoni mwa vijana mashoga Thailand yaongezeka

Picha: UNICEF/Thailand

Maambukizi ya HIV miongoni mwa vijana mashoga Thailand yaongezeka

Kiwango cha maambukizi mapya ya virusi vya Ukimwi, nchini Thailand kinaripotiwa kuongezeka miongoni mwa vijana wa kiume wanaojihusisha na mapenzi ya jinsia moja.

Ripoti iliyotolewa na shirika la Umoja wa Mataifa linalohusika na watoto UNICEF inasema kuwa maambukizi hayo yamejitokeza zaidi kwa vijana wenye umri wa kuanzia miaka 15 hadi 24.

Miongoni mwa sababu ya ongezeko hilo ni vijana hao kushiriki mapenzi ya jinsia moja, vijana kuuza miili yao na kujihusisha na matumizi ya madawa ya kulevya kwa njia ya kujidunga sindano.

Mkuu wa kitengo cha Ukimwi cha UNICEF nchini humo Robert Gass amesema kuwa ukosefu wa stadi za maisha katika mazingira hatarishi na matumizi ya pombe na dawa za kulevya huweka vijana katika mazingira hatari ya kupata HIV na magonjwa na zinaa.

UNICEF imesema inaamini kuwa Thailand inahitaji hatua za haraka za kulinda vijana kwani vijana wenye uhusiano wa karibu na familia zao wana uwezekano mdogo wa kutumbukia kwenye hatari za kupata Ukimwi kuliko wale wasio na uhusiano wa aina hiyo.