Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mali: Ban alaani mauaji ya walinda amani wawili

Walinda amani katika doria maeneo ya Ber, Timbuktu, Mali. Picha ya MINUSMA

Mali: Ban alaani mauaji ya walinda amani wawili

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki Moon amelaani vikali shambulio la kujitoa muhanga lililotokea Mali, maeneo ya Timbuktu asubuhi hii dhidi ya kituo cha Umoja wa Mataifa nchini humo, MINUSMA na kusababisha vifo vya walinda amani wawili pamoja na majeruhi saba.

Bwana Ban ameeleza kusikitishwa sana na mauaji ya walinda amani hawa, akipeleka rambirambi zake kwa familia za wahanga na kuwatakia nafuu waliojeruhiwa.

Amesema, mashambulizi haya hayatazuia Umoja wa Mataifa kuendelea na juhudi zake za kusaidia raia wa Mali kupata amani nchini humo.

Hali ya usalama kaskazini mwa Mali imezidi kuzorota tangu mwanzo wa mwaka huu, lakini makubaliano ya amani yalisainiwa mwezi Mei, na mazungumzo yanaendelea mwezi huu ili kupata suluhu ya kisiasa ya mzozo huo.

Wakati huo huo, mashirika ya kibinadamu yametoa wito kwa ufadhili ili kupambana na ukosefu wa usalama wa chakula unaokumba Mali, pamoja na changamoto kadhaa zinazosababishwa na ugaidi, ukame na idadi ya wakimbizi inayoongezeka kutoka nchi jirani za Jamhuri ya Afrika ya Kati na Nigeria.