Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kamati ya UM yajadili uenezaji ugaidi katika taasisi za elimu

UN Photo/Paulo Filgueiras
Mkutano wa Halmashauri ya Kamati ya Baraza la Usalama ya Kukabiliana na Ugaidi, CTED. Picha:

Kamati ya UM yajadili uenezaji ugaidi katika taasisi za elimu

Halmashauri ya Kamati ya Baraza la Usalama ya Kukabiliana na Ugaidi, CTED, ikishirikiana na Wakfu wa Imani wa Tony Blair, imekuwa na mdahalo leo kuhusu mchango wa elimu katika kukabiliana na misimamo mikali inayoeneza ukatili wa kigaidi.

Miongoni mwa yaliyokuwa kwenye ajenda ya mdahalo huo ni pamoja na jinsi ya kutekeleza azimio namba 1624 (2005) la Baraza la Usalama kuhusu mbinu za kina za kupambana na ugaidi na uelewa wa hatari ya kutumiwa kwa taasisi za elimu na magaidi na wafuasi wao katika kueneza kasumba ya ugaidi, kama ilivyobainishwa kwenye azimio hilo namba 1624.

Halikadhalika, mjadala huo umeangazia njia mwafaka zinazoweza kuchukuliwa na nchi wanachama kukabiliana na hatari hizo, kwa kuendeleza programu za elimu zinazochagiza maelewano baina ya tamaduni tofauti na kuvumiliana, pamoja na sera mathubuti na mapendekezo ya usaidizi unaoweza kutolewa na Umoja wa Mataifa kwa nchi wanachama ili kupunguza hatari ya kutumia taasisi za elimu kueneza kasumba ya ugaidi.