Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Nchi zakumbushwa kuhusu wajibu wa kulinda sheria ya kimataifa

UN Photo/Paulo Filgueiras
UN Photo/Paulo Filgueiras

Nchi zakumbushwa kuhusu wajibu wa kulinda sheria ya kimataifa

Rais wa Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu, ICC, Sang Hyun Song, ameziomba nchi zote duniani zishirikiane kupambana na ukwepaji wa sheria, ikiwa leo ni siku ya sheria ya kimataifa duniani.

Taarifa kamili na Amina Hassan.

Raisi Sang Hyun Song amekumbusha kwamba, tarehe 17, Julai, mwaka 1998, nchi 120 zilitia saini kwenye maktaba wa Roma uliounda ICC, ambayo ni mahakama ya kwanza inayodumu na inayolenga kufuatilia uhalifu wa kibinadamu na mauaji ya kimbari, akisema:

“ Tukiadhimisha siku ya Julai, tarehe 17, tunatambua juhudi zilizofanyika kukuza maridhiano kwenye jamii mbalimbali duniani na zilizobadili maisha ya maelfu ya waathiriwa. Tunatizama pia mustakhabali wetu, tukirudia utashi wa jamii ya kimataifa katika kupambana na ukwepaji wa sheria kuhusu mauaji mabaya zaidi na kuhakikisha hayatokei tena”

Ameongeza kwamba wote wanafahamu kasoro za ICC, na ni lazima kuendelea kujitahidi ili mkataba wake uridhiwe na mataifa yote duniani, lakini pia, amesisitiza kwamba ni jukumu la kila nchi na kila mtu kuhakikisha sheria za kimataifa zinaheshimiwa kote duniani.