Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Wakimbizi wa Syria hatarini wakati ufadhili ukididimia

Wakimbizi wa Syria hatarini wakati ufadhili ukididimia

 Hali ya kibinadamu ya wakimbizi wa Syria huenda ikazorota zaidi katika miezi michache ijayo wakati mashirika ya misaada yakikabiliwa na ugumu wa kupata fedha za kukidhi mahitaji yanayoongezeka, kwa mujibu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi, UNHCR.

 UNHCR imesema kuwa idadi ya wakimbizi katika ukanda mzima inatazamiwa kuongezeka hadi milioni 3.6 ifikapo mwishoni mwa mwaka huu, ikionya kuwa uhaba wa ufadhili huenda ukaongeza madhila na hatari zinazowakabili wakimbizi hao.

 Akizungumza na Patrick Maigwa wa Radio ya Umoja wa Mataifa leo mjini Geneva, msemaji wa UNHCR Adrian Edwards amesema

 “ Tunahitaji dola bilioni 3.7 mwaka huu kwa mahitaji ya nchi jirani za Syria zinazopokea wakimbizi. Kwa sasa tumekusanya asilimia 30 ya kiasi hicho, kwa hiyo unaona kuna pengo kubwa katika sehemu tulipo sasa katikati ya 2014 na sehemu tunapotaka kufikia”

 Ameongeza, kushindwa kutoa msaada wa kibinadamu wa kutosha  kwa wakimbizi wa Syria kufikia mwisho wa mwaka huu wa 2014, kunaweza kuchangia madhara makubwa kwa wakimbizi hao huku akizitaja:

 “  Hatari zaidi ya kutofikia watu, hatari ya kuongezeka kwa utapiamlo, shida nyingi kutokana na watoto kutoandikiswa shuleni, na hatari nyingine kubwa ni kuzorotesha hali ya utulivu ya ukanda mzima, tukishindwa kupeleka misaada ya kibinadamu”