Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kikao cha Baraza la Mazingira chahitimishwa Nairobi

Kikao cha Baraza la Mazingira chahitimishwa Nairobi

Kikao cha utangulizi cha Baraza la Mazingira la Umoja wa Mataifa kimehitimishwa leo mjini Nairobi Kenya, huku mawaziri wanawake wakikutana na viongozi katika sekta ya mazingira kujadili jinsi ya kulijumuisha suala la jinsia katika agenda ya mazingira. Assumpta Massoi na taarifa kamili

Taarifa ya Assumpta

Mikutano ya wiki nzima ya Baraza la Mazingira ililenga kutoa kipaumbele kwa suala la mazingira katika ajenda ya kimataifa kuhusu maendeleo endelevu. Masuala kadhaa yamekuwa yakimulikwa, yakiwemo kukabiliana na ujangili na biashara haramu ya viumbe wa pori, ufadhili wa mikakati inayoendeleza uwekezaji unaojali mazingira, pamoja na uchafuzi wa mazingira.

Hii leo kabla ya kutamatisha vikao vya Baraza hilo la Mazingira, kumefanyika mkutano wa mtandao wa mawaziri wanawake na viongozi katika mazingira, ambao ulijikita katika kulijumuisha suala la jinsia katika utungaji sera kuhusu mazingira na ajenda ya maendeleo endelevu.

Mmoja wa washiriki wa mkutano huo alikuwa Bi. Lisa Emilia Svensoon, Balaozi wa bahari na Maji safi wa Sweden, akizungumzia udhibiti wa mabahari na mabadiliko ya tabianchi

“Mara nyingi katika mikutano kuhusu bahari, masuala ya wanawake hayazungumzwi, na wakati mwingine hata wanawake hawashiriki katika mikutano hiyo. Ukizingatia uhakika wa kuwa na chakula, watu bilioni moja wanategemea protini kutoka baharini, na wengi wao ni wanawake.”