Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Watu zaidi wakimbia makwao Sudan Kusini, licha ya makubaliano ya kusitisha mapigano

Mtoto akiwa kambini Tomping Juba, Sudan Kusini. Picha ya UM/Eskinder Debebe

Watu zaidi wakimbia makwao Sudan Kusini, licha ya makubaliano ya kusitisha mapigano

Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi, UNHCR, limesema kuwa idadi ya ya watu wanaokimbia mapigano nchini Sudan Kusini imeendelea kuongezeka katika kipindi cha takriban wiki tatu tangu kutiwa saini makubaliano ya kusitisha mapigano mjini Addis Ababa, mnamo Mei 9.

Idadi ya watu waliolazimika kuhama makwao ndani mwa Sudan imepanda kwa watu 46,000 na hivyo kufikisha idadi ya wakimbizi wa ndani milioni moja na elfu tano. Katika kipindi hicho, idadi ya wakimbizi wa Sudan Kusini katika nchi za Ethiopia, Kenya, Sudan na Uganda imepanda kwa zaidi ya watu 20,000 na kufikia 370,000.

Adrian Edwards ni msemaji wa UNHCR

Sudan Kusini imenaswa katika mgogoro huu kwa zaidi ya miezi sita, na kuifanya hali ngumu tayari ya kibinadamu kuwa hata mbaya zaidi. Makubaliano yaliyosainiwa mwezi Mei yalikuwa ya pili. Ethiopia inatoa makao kwa idadi kubwa zaidi ya wakimbizi, wakiwa ni zaidi ya 131,000, na wengi wao wakiwa wanawake na watoto.”

Bwana Edwards amesema wakimbizi waliowasili karibuni wanasema wamekimbia mapigano katika majimbo ya Jonglei na Upper Nile, yaliyoko karibu na Ethiopia, hususan maeneo ya Mathiang na Longechuk jimbo la Upper Nile.

Wale watokao maeneo mengine walisema wanahofia mashambulizi hivi karibuni na uhaba wa chakula. Ili kuwapa makazi wakimbizi hao, UNHCR na mamlaka za Ethiopia zimefungua kambi tatu mpya mwaka huu 2014, mbili zikiwa zimejaa tayaru, kwa idadi ya watu 95, 085.”