Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Amos kuhusu Syria: Nimetoa shuhuda na mapendekezo sasa Baraza ndio la kuchukua hatua:

Amos kuhusu Syria: Nimetoa shuhuda na mapendekezo sasa Baraza ndio la kuchukua hatua:

Ni miezi miwili sasa tangu azimio nambari 2319 la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kupitishwa kuhusu Syria lakini bado hali ni mbaya nchini humo, amesema Valerie Amos Mkuu wa masuala ya usaidizi wa binadamu kwenye Umoja wa Mataifa katika sentensi yake ya ufunguzi alipozungumza na waandishi wa habari baada ya kuhutubia Baraza la Usalama siku ya Jumatano.

Bi. Amos amesema amewaeleza wajumbe kuwa kuna maendeleo madogo tangu ahutubie baraza hilo.

(Amos)

“Hakika niliwaambia kwamba kila mwezi ninatoa ripoti kuhusu mauaji na ukatili dhidi ya raia, kuharibiwa kwa makazi, shule na maeneo ya ibada. Kutothaminiwa kwa maisha na kutojali kwa pande husika ni ukiukwaji jumla wa sheria za kimatiafa.”

Akaenda mbali zaidi kueleza kuwa hatua zinazochukuliwa sasa kusuluhisha mzozo huo zimekuwa na mafanikio madogo sana na baadhi ya misingi ya Umoja wa Mataifa inayotumika katika utendaji wake inakiukwa kila siku nchini Syria.

(Amos)

Nchini Syria misingi hiyo ya maadili na wajibu wa serikali wa kulinda wananchi  vinakiukwa kila siku. Nadhani sasa jukumu limo mikononi mwa Baraza hili sio tu kutambua uhalisia huo bali pia kuchukua hatua.”

Mwandishi mmoja wa habari akamuuliza Mkuu huyo wa OCHA kwani asitake wahusika wawajibishwe kutokana na madhila aliyoshuhudia na ripoti zinazoibuliwa juu ya kile kinachoendelea Syria.

(Amos)

Aah siidhani kama ninaweza kuwa na uthabiti zaidi kwenye taarifa nilizotoa kwa baraza la usalama na ushahidi niliopatia baraza juu ya ukiukwaji wa kupindukia wa sheria za kimataifa kuhusu haki za binadamu bali pia suala kwamba azimio lenye la baraza la usalama linakiukwa.”