Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Idadi ya wakimbizi wa ndani huko Katanga, DRC yafikia 500,000

Idadi ya wakimbizi wa ndani huko Katanga, DRC yafikia 500,000

Mashirika ya usaidizi wa kibinadamu nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC yameripoti kuwa idadi ya watu waliopoteza makazi tangu kuanza kwa mwaka huu kwenye jimbo la Katanga nchini humo imeongezeka na kufikia Laki Tano.

Msemaji wa Umoja wa Mataifa, Stephane Dujarric amesema ongezeko hilo linatokana na watu wapya 100 waliokimbia makazi yao tangu kuanza kwa mwaka huu pekee kutokana na mapigano kati ya majeshi ya serikali na vikundi vilivyojihami kwenye kwenye jimbo hilo.

Mashirika hayo yanasema ukosefu huo wa usalama unakwamisha shughuli za kilimo na hata zile za afya.

(Sauti ya Dujarric)

Ukosefu wa usalama unaathiri pia uzalishaji wa chakula na kufika kwenye masoko na hivyo kuacha zaidi ya asilimia 80 ya wakimbizi wa ndani bila uhakika wa chakula. Katika miezi mitatu ay kwanza ya mwaka 2014, shirika la mpango wa chakula duniani lilipatia msaada wa chakula karibu watu 70,000. UNICEF na WHO na wadau nao wanatoa msaada wa kinga dhidi ya Kipindupindu kutokana na wagonjwa 3500 waliopatikana kwenye jimbo hilo tangu mwezi Januari. Kampeni ya hivi karibuni ya chanjo dhidi ya surua pia imelenga zaidi ya watoto Milioni Saba walio na umri wa chini ya miaka Kumi.”