Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Palestina yaomba kuungana na mikataba ya UM

Palestina yaomba kuungana na mikataba ya UM

Mwakilishi wa Umoja wa Mataifa amesema kwamba Umoja wa Mataifa umepokea rasmi maombi ya Palestina kuungana na mikataba tofauti 15, ikiwemo mikataba ya The Hague na ya Geneva kuhusu sheria na kanuni za vita, na pia mikataka mingine kama vile juu ya haki za watoto vitani au dhidi ya ubaguzi.

Mwakilishi huyu ameongeza kwamba Umoja wa Mataifa utayaangalia haya maombi, na kuamua hatua za kuchukua. Amerejelea matarajio ya Umoja wa Mataifa kuendelea na harakati za amani kati ya Israel na Palestina.

Akizungumza mbele ya waandishi wa habari mjini New York, Balozi wa Palestina katika Umoja wa Mataifa, Riyad Mansour, amewakumbusha kwamba tangu Novemba mwaka 2012, Baraza Kuu limeipatia Palestina hadhi ya uangalizi bila haki ya kupiga kura.

(Sauti ya Mansour)

“Tunatumia haki yetu ya kisheria, kama nchi inayostahili kuungana na mbinu hizi. Sisi ni binadamu, na hatua hiyo itatusaidia kutekeleza sheria zilizoandaliwa na mikataba hii.Tunajisifia na hilo, tumefurahi, na tunaangalia hatua iliyochukuliwa na rais wetu kama njia ya kuimarisha nguzo za nchi ya Palestina katika jamii ya kimataifa”.  

Bwana Mansour ameendelea kwa kushukuru wanaosaidia harakati za amani kati ya Israel na Palestina, akiongeza kwamba Palestina iko tayari kuendela na mazungumzo ili kufikisha mwelewano na kutekeleza suluhu la kukubalia nchi mbili.