Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ban ataka hatua madhubuti kuelekea mkutano wa kilele kuhusu hali ya hewa

Ban ataka hatua madhubuti kuelekea mkutano wa kilele kuhusu hali ya hewa

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-Moon ametaka mataifa yote duniani kutangaza hatua za haraka na za kijasiri kuelekea mkutano wa hali ya hewa mwezi Septemba mwaka huu kwa kuzingatia ripoti mpya ya mabadiliko ya tabianchi.

Bwana Ban amekaririwa na msemaji wake akieleza kuwa ripoti iliyotolewa huko Japan na kikundi kazi cha jopo la kimataifa la hali ya hewa, IPCC imeeleza dhahiri shahiri kuwa udhibiti wa mabadiliko ya tabianchi utakuwa mgumu iwapo viwango vya joto vitazidi kuongezeka.

Kwa mantiki hiyo ametaka mikakati ya kijasiri ya kuwezesha kupunguza viwango vya gesi chafuzi duniani na kuweka maandalizi ya kukabiliana na majanga yatokanayo na mabadiliko ya tabianchi.

Halikadhalika Ban ametaka kila liwezekanalo lifanyike kufikia makubaliano kuhusu mabadiliko ya tabianchi ifikapo mwaka 2015.