Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mabadiliko ya tabianchi ni dhahiri, tuchukue hatua: Ban asema hayo huko Greenland

Mabadiliko ya tabianchi ni dhahiri, tuchukue hatua: Ban asema hayo huko Greenland

Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa aliyeko ziarani huko Greenland ameeleza wasiwasi wake juu ya kasi ya kuyeyuka kwa barafu kwenye nchi hiyo iliyofunikwa kwa barafu na theluji.

Akizungumza mjini Ummannag katika mkutano na waandishi wa habari uliohudhuriwa pia na Waziri Mkuu wa Denmark, Aleqa Hammond, Bwana Ban amesema pamoja na kuvutiwa na ukaribu na uzuri wa mji bado mabadiliko ya tabianchi yanatishia siyo tu uwepo wa eneo hilo bali pia maeneo mengine duniani.

Kwa mantiki hiyo ametaka hatua za pamoja na za haraka kuchukuliwa ili kulinda mazingira ya nchi hiyo yaliyo tegemeo kwa vizazi vilivyoishi eneo hilo kwa maelfu ya miaka na mazingira yaliyo bora.

Amesema kunaweza kuwepo na umuhimu wa kufanya tafiti zaidi kuhusu athari za mabadiliko ya tabianchi lakini ukweli ni kwamba mabadiliko hayo yapo na athari zake ni za kasi kuliko inavyodhaniwa.

Bwana Ban amesema ni kutokana na hali hiyo ameamua kuitisha kikao kuhusu mabadiliko ya tabianchi mwezi Septemba mwaka huu mjini New York ili kuchagiza kasi ya kukabiliana na mabadiliko hayo.

Amesema ni matumaini yake kuwa viongozi watashiriki mkutano huo na kuonyesha utashi wa kisiasa kuokoa sayari ya dunia ili vizazi vijavyo viweze kuishi katika mazingira endelevu.