Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

UM wawakumbusha raia wa Afghanistan kuhusu uhuru wao kupiga kura

UM wawakumbusha raia wa Afghanistan kuhusu uhuru wao kupiga kura

Huku zikiwa zimesalia siku 23 kabla ya uchaguzi wa rais na wanachama wa mabaraza ya mikoa nchini Afghanistan, ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini humo, UNAMA, umesisitiza kuwa kushiriki kupiga kura ni haki ya kimsingi ya kila mtu.

Mwakilishi wa Katibu Mkuu na Mkuu wa UNAMA, Ján Kubiš, amesema, kama watu kwingineko kote duniani, wanaume na wanawake wa Afghanistan wana haki ya kuichagua serikali na viongozi wao bila vitisho, akiongeza kuwa kushiriki kwao ni muhimu hasa wakati wa uchaguzi huu wa kihistoria ambao utaweka njia mpya ya mustakhbali wa Afghanistan.

Uchaguzi wa rais na Baraza la Mikoa umepangwa kufanyika mnamo Aprili 5, 2014. Bwana Kubiš amewakumbusha raia wa Afghanistan kwamba katiba ya nchi yao inasema kuwa wananchi wote wana haki ya kuchagua na kuchaguliwa, na kwamba taifa lao pia lilipiga kura ya kupitisha Azimio la Kimataifa la Haki za Binadamu la Mwaka 1948.