Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mkutano kuhusu mabadiliko ya tabianchi waanza leo Bonn, Ujerumani

Mkutano kuhusu mabadiliko ya tabianchi waanza leo Bonn, Ujerumani

Huko Bonn, Ujerumani hii leo kunaanza mashauriano ya kwanza kabisa kwa mwaka huu kuhusu mabadiliko ya tabianchi, mashauriano ambayo yatarajiwa kuwezesha kufikia makubaliano ya dhati kuhusu mabadiliko ya tabianchi baadaye mwakani huko Paris.

Taarifa ya kamati ya Umoja wa Mataifa kuhusu mkataba wa kimataifa wa mabadiliko ya tabianchi, UNFCCC inasema kuwa mashauriano hayo ya wiki moja yanajikita kwenye mpango utekelezaji wa Durban utakaowezesha makubaliano mapya yanayotarajiwa kuanza kutekelezwa mwaka 2020.

Ahadi ambazo hadi sasa mataifa yametoa ili kupunguza viwango vya gesi chafuzi ni asilimia 80 tu ya viwango vya gesi hizo duniani nzima, hata hivyo UNFCCC inasema  licha ya kwamba kiwango hicho kinatia moyo bado ni pungufu ya punguzo linalohitajika ili kiwango cha joto duniani kiweze kupungua angalau kwa nyuzi joto 2 za Selsiyasi.

Maudhui ya mkutano huo ni nishati yenye tija na nishati asilia huku UNFCCC ikieleza kuwa mikutano mingine itakayofuatia itakuwa na maudhui mengine.