Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Asilimia 95 ya wapiga kura wamejiandikisha Guinea-Bissau

Asilimia 95 ya wapiga kura wamejiandikisha Guinea-Bissau

Wakati Guinea-Bissau ikijiandaa kwa ajili ya uchaguzi wa Rais na wabunge mwezi Aprili mwaka huu, mjumbe maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa nchini humo José Ramos-Horta amesema takribani asilimia 95 ya watu wanaostahili kupiga kura wamejiandikisha.

Bwana Ramos-Horta ameliambia Baraza la Usalama hii leo kuwa kwenye kinyang’anyiro cha uchaguzi wa Urais kuna wagombea 12 ilhali vyama 40 vya siasa vinatarajiwa kushiriki kuwania ubunge. Amesema tarehe 10 mwezi huu serikali ilitangaza kuhitimishwa kwa kazi ya kuandikisha wapiga kura.

(Sauti ya Ramos)

"Inatarajia kuwa orodha ya mwisho ya wapiga kura itakuwa tayari mwishoni mwa wiki ijayo. Yakadiriwa watu Laki Saba na Elfu Sabini wamejiandikisha kupiga kura hii ni takribani asilimia 95 ya wale wote 810,961 wenye haki ya kupiga kura. Hii ni rekodi ya aina yake.”

Bwana Ramos-Horta anaongoza ofisi ya Umoja wa Mataifa ya kusaidia ujenzi wa Guinea-Bissau iliyoanzishwa mwaka 2009 kusaidia nchi hiyo katika harakati za kujijenga. Guinea-Bissau ilipata uhuru wake kutoka Ureno mwaka 1974 na imekuwa ikikumbwa na mapinduzi ya kijeshi na ukosefu wa utulivu wa kisiasa.