Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mkuu wa UNHCR Guterres asikitishwa na hali CAR

Mkuu wa UNHCR Guterres asikitishwa na hali CAR

Kamishna Mkuu wa Shirika la Kuhudumia Wakimbizi katika Umoja wa Mataifa, Antonio Guterres, amesema kuwa amesikitishwa mno na hali nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati, ambako amesema ameshuhudia janga la kibinadamu la kiwango kisichoelezeka.

Bwana Guterres amesema mauaji ya uangamizaji wa kikabila na kidini yanaendelea, pamoja na mauaji ya kiholela ya halaiki.

Amesema kuwa makumi ya maelfu ya watu wamekuwa wakiikimbia nchi yao kwa ajili ya usalama wao, huku wengine wakiwa wamenaswa bila kujua pa kuenda.

Mkuu huyo wa UNHCR ameongeza kuwa, hata baada ya kuteuliwa rais mpya na serikali mpya, bado serikali hiyo haina uwezo wa kuwalinda raia kikamilifu. Ametoa wito kwa jamii ya kimataifa kushirikiana ili kuongeza vikosi vya kuweka utulivu na polisi nchini humo, kwani usalama ndicho kitu cha kipaumbele kwa raia wa Jamhuri ya Afrika ya Kati.