Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ufugaji wa samaki kuwa mkombozi ifikapo mwaka 2030

Ufugaji wa samaki kuwa mkombozi ifikapo mwaka 2030

Ripoti mpya ya mashirika ya Umoja wa Mataifa imeweka bayaan kuwa ufugaji wa samaki utachangia karibu theluthi mbili ya kitoweo cha samaki duniani ifikapo mwaka 2030. Benki ya dunia, Shirika la chakula na kilimo duniani FAO na lile la kimataifa la utafiti wa sera za chakula yamesema hali hiyo inatokana na kupungua kwa samaki wanaovuliwa kwenye vyanzo asilia na ongezeko la watu wa tabaka la kati nchini China.

Mathalani ifikapo mwaka 2030 soko kuu la samaki litakuwa ni China ikitumia asilimia 38 ya samaki wote kwenye soko na ndio maana nchi hiyo na nyinginezo zimeamua kuwekeza kwenye ufugaji samaki ili kukidhi mahitaji ,Siwa Msangi ambaye ni mmoja wa waandishi wa ripoti hiyo amesema wamebaini kuwa ufugaji samaki utaimarika zaidi kuliko ilivyodhaniwa hapo awali.

Hata hivyo Mkurugenzi wa huduma za kilimo na mazingira kutoka Benki ya dunia Juergen Voegele amesema ripoti inatoa taarifa njema kwa nchi zinazoendelea jinsi ya kutumia uvuvi kukuza uchumi lakini suala muhimu ni kuweka sera endelevu ili kuhakikisha rasilimali hiyo inatumika vyema.