Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Hukumu dhidi ya Katanga yasogezwa mbele mwezi mmoja

Hukumu dhidi ya Katanga yasogezwa mbele mwezi mmoja

Mahakama ya Kimataifa ya  makosa ya jinai, ICC  huko The Hague, Uholanzi imesogeza mbele kwa mwezi mmoja zaidi tarehe ya kusomwa hukumu dhidi ya Germain Katanga kutokana na mmoja wa majaji kupata udhuru wa kiafya.

Taarifa ya ICC imesema hukumu hiyo ilikuwa isomwe Ijumaa hii tarehe Saba lakini sasa itasomwa tarehe Saba mwezi ujao.

Katanga anayedaiwa kuwa kamanda wa kikosi cha FPRI huko Ituri Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC alishtakiwa kwa makosa kumi, ikiwemo matatu ya uhalifu dhidi ya binadamu yakijumuisha ubakaji na mauaji.

Makosa mengine saba ni ya uhalifu wa kivita yakihusisha kutumikisha watoto wenye umri wa chini ya miaka 15 na kuelekeza mashambulizi kwa raia.

Kesi yake ilianza kusikilizwa tarehe 24 Novemba mwaka 2009 na kwa sasa yuko mikononi mwa mahakama.