Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Katibu Mkuu awasili Ujerumani, kuwa na mazungumzo na viongozi

Katibu Mkuu awasili Ujerumani, kuwa na mazungumzo na viongozi

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-Moon amewasili Berlin nchini Ujerumani ambako tayari amekuwa na mazungumzo na Waziri wa Mambo ya Ndani Thomas de Maizière na kesho atakuwa na mazungumzo na Rais Joachim Gauck pamoja na Kansela Angela Markel.

Ziara ya Bwana Ban huko Ujerumani inafuatia ile ya Cuba ambako akiwa nchini humo alihudhuria mkutano wa viongozi jumuiya ya nchi za Amerika Kusini na Karibeani, CELAC.

Bwana Ban alisifu nchi hizo kwa sera zao za kipekee za kuimarisha hifadhi ya kijamii, afya na elimu akisema kuwa ni mfano wa kuigwa duniani kote.

Amesema kwa upande wake Umoja wa Mataifa utaendelea kuunga mkono jitihada za ukanda huo kuweka maendeleo jumuishi kupitia tume ya uchumi ya Umoja wa Mataifa kwa nchi za Amerika Kusini na Karibean kama vile ambavyo nchi hizo zinachangia maendeleo ya dunia nzima.