Sudan Kusini wakubaliana kusitisha mapigano, Ban apongeza
Hatimaye pande zinazopingana huko Sudan Kusini zimetia saini makubaliano ya kusitisha mapigano yaliyoanza nchini humo tarehe 15 Disemba mwaka jana, hatua ambayo imekaribishwa vyema na Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-Moon.
Akizungumza mjini Davos wakati akiwa kwenye shughuli ya shirika la mpango wa chakula duniani, WFP kuhusu kutokomeza njaa, Bwana Ban amesema habari hizo zimemtia sana moyo kwani Sudan Kusini wamekuwa na mapigano ya wenyewe kwa wenyewe na sasa wametia saini makubaliano ya kusitisha mapigano huko Addis Ababa chini ya uratibu wa IGAD.
Amesema Umoja wa Mataifa umekuwa ukishiriki vyema kwenye harakati za kufikai mpango huo na ni matumaini yake kuwa makubaliano hayo yatatoa fursa bora kwa wananchi na hata kwa Umoja wa Mataifa kuweza kuelekeza rasilimali na muda kwenye maeneo mengine ya usaidizi wa binadamu kama vile kutokomeza njaa.