Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Pande mbili husika, mzozo wa Syria zakutana ana kwa ana Uswizi

Pande mbili husika, mzozo wa Syria zakutana ana kwa ana Uswizi

Kongamano la kimataifa linalolenga kuumaliza mzozo uliopo nchini Syria umefunguliwa leo mjini Montreux Uswisi leo Jumatano huku wito ukitolewa kwa pande zote kujitoa kwa mazungumzo yakinifu ili kumaliza takriban miaka mitatu ya ghasia. George Njogopa na taarifa kamili

 (TAARIFA YA GEORGE NJOGOPA)

Katibu Mkuu Ban Ki-moon ameelezea mapigano yanayoendelea nchini Syria kama vita vilivyopindukia ambavyo vinaendelea kusababisha mamia ya watu kupoteza maisha.

Amesema kuwa zaidi ya watu 100,000 wamepoteza maisha huku wengine zaidi ya milioni 9.5 wakikosa makazi na kuwa katika mahitaji ya dharura.

Katibu huyo ameeleza kuwa jamii ya Wasyria ndiyo wenye wajibu wa kumaliza mapigano hayo kiwa kwa kutekeleza maazimio yaliyofikiwa Geneva hapo mwaka 2012.

Ban ameitolea mwito pia jumuiya ya kimataifa kuendelea kuiunga mkono Syria ili kufanikisha majadiliano yanayoendelea kwa shabaha ya kuleta mustakabala mwema wa taifa hilo.

 “Baada ya takribani ya miaka mitatu ya machafuko na maumivu huko Syria, leo ni siku tete lakini yenye matumaini makubwa. Kwa mara ya kwanza, Serikali ya Syria na wapinzani wa Syria, nchi za kieneo na jumuiya ya kimataifa kwa pamoja wanakutana kwa ajili ya kusaka suluhu ya kisiasa kwa vifo, uhalibifu na uliojitokeza nchini humo. Tamko la pamoja la Geneva linafafanua hatua muhimu kwa kipindi cha mpito nchini Syria, ikianza na kuundwa kwa chombo cha mpito chenye  madaraka kamili yalioafikiwa na pande zote ikiwemo kuhusu mamlaka ya vikosi vya jeshi, Usalama na Upelelezi”