Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ban akaribisha matokeo ya uchaguzi Madagascar

Ban akaribisha matokeo ya uchaguzi Madagascar

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon Jumamosi amekaribisha matokeo ya mwisho ya uchaguzi wa Rais nchini Madagascar yaliyothibitishwa na ambayo waangalizi wa kimataifa wametoa tathimini na kusema uchaguzi ulifanyika kwa amani na utaratibu uliotakiwa.

Ban ametoa wito kwa wagombea wote kukubali uamuzi wa mahakama maalumu ya uchaguzi kwa kutoa malalamiko yao kwa amani kupitia vyombo vya kisheria. Kufuatia uchuguzi huo uliokuwa na ushindani mkali Katibu Mkuu ameutolea wito uongozi mpya kuzungumza na upande wa upinzani na kuongoza nchi hiyo kwa maslahi ya raia wote.

Ban amewachagiza viongozi wa kisiasa na taasisi za serikali kufanya kazi pamoja kuelekea maridhiano , demokrasia na kujiinua tena kiuchumi. Ameongezsa kuwa Umoja wa Mataifa utaendelea kuunga mkono mchakato wa maendeleo nchini Madagascar.