Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Nilichoshuhudia Sudan Kusini kinatisha: Šimonović

Nilichoshuhudia Sudan Kusini kinatisha: Šimonović

Msaidizi wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kwa masuala ya haki za binadamu, Ivan Šimonović amehitimisha ziara yake ya siku nne huko Sudan Kusini na kusema kwa ujumla hali inatisha na pande zote kwenye mzozo huo zimefanya mauaji ya kutisha.

Akizungumza mjini Juba, Šimonović amesema ziara yake ilimpeleka Juba mji mkuu wa Sudan Kusini, Bor huko Jonglei na Bentiu jimbo la Unity ambako kuna uharibifu mkubwa wamali, mauaji kinyume cha sheria na miili ya watu imetapakaa hovyo barabarani.

(Sauti ya Šimonović)

Amesema mwezi Mmoja wa mapigano umerejesha nyuma Sudan Kusini kwa muongo mmoja na kilichotokea ni kichocheo cha kuundwa kwa tume huru ya uchunguzi ili kufahamu ukweli halisi.

Wakati wa ziara hiyo alikuwa na mazungumzo na viongozi wa serikali na vikundi vya upinzani.

Nalo shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto UNICEF, limesema lina taarifa kuwa watoto wameanza kutumika jeshini huko Sudan Kusini jambo ambalo ni kinyume na sheria za kimataifa.