Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ban asikitishwa na vifo nchini Bangladesh, atoa wito kwa vyama vya siasa

Ban asikitishwa na vifo nchini Bangladesh, atoa wito kwa vyama vya siasa

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon ameeleza kusikitishwa kwake na vifo vilivyotokea nchini Bangladesh pamoja na matukio ya vurugu wakati wa uchaguzi wa wabunge siku ya jumapili, uchaguzi ambao amesema ulighubikwa na mvutano na ushiriki wa wapiga kura ulikuwa ni mdogo.

Ameeleza masikitiko yake kuwa vyama husika vilishindwa kuafikiana juu ya mambo ambayo yangaliweza kufanya uchaguzi huo kuwa wa amani na hata matokeo yake kuwa jumuishi.

Katibu Mkuu ametaka pande zote kujizuia na kuhakikisha wanapatia kipaumbele suala la amani na kuweka mazingira stahili kwa watu kushiriki mikutano na hata kujieleza. Amesema ghasia na mashambulizi dhidi ya raia haviwezi kukubalika.

Kuhusu vyama vya siasa amevitaka virejelee mashauriano yenye maana na kushughulikia haraka matarajio ya wananchi wa Bangladesh ya kuwa na mchakato jumuishi wa kisiasa. Amesema Umoja wa Mataifa kwa upande wake utaendelea kusaidia nchi hiyo kwenye mchakato wake wa kidemokrasia kwa mujibu wa misingi ya ujumuishi, kuepuka ghasia, mashauriano na maridhiano.