Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Watu 200,000 wakimbia makwao Sudan Kusini, misaada yaongezwa : OCHA

Watu 200,000 wakimbia makwao Sudan Kusini, misaada yaongezwa : OCHA

Taarifa iliyotolewa Ijumaa na mratibu wa masuala ya kibinadamu nchini Sudan Kusini Toby Lanzer inasema machafuko nchini Sudan Kusini yamewafungisha virago na kuwalazimu kuhama makwao takriban watu 200,000 katika wiki mbili zilizopita na kuathiri maelfu ya wengine. Assumpta Massoi na maelezo kamili

(TAARIFA YA ASSUMPTA MASSOI)

Kwa mujibu wa shirika la Umoja wa mataifa la kuratibu misaada ya kibinadamu OCHA mashirika mbalimbali ya misaada yanaongeza juhudi hususani katika miji ambayo imeathirika saana na machafuko na maeneo ya vijijini ambako raia wamekimbilia kupata usalama. Idadi kubwa ya raia wako Awerial, na jilo la Lakes ambako imeelezwa watu 76,000 wamekusanyika pamoja. 

OCHA inasema mashirika ya misaada yanagawa chakula, vifaa visivyo chakula na huduma za msingi za afya kwa watu hao, huku yalkijitahidi kupatikana kwa maji safi na huduma ya maliwato. Bwana Lanzer ametoa wito kwa pande zote kuyasaidia mashirika ya misaada kupata fursa ya kuwafikia raia na kulinda na kuheshimu shughuli za kibinadamu, wafanyakazi wa misaada na mali zao kila wakati. Yens Laerke ni msemaji wa OCHA

 (SAUTI YA JENS LAERKE)

"Idadi kubwa ya raia wanaohitaji msaada iko Awerial, jimbo la Lakes ,ambako watu  76,000sasa wamekusanyika na mashirika ya misaada yanagawa chakula na vifaa visivyo vya chakula pamoja na huduma za msingi za afya. Katika siku zijazo tunaongeza operesheni zetu na pia tutahakikisha kuna maji safi na huduma za vyoo kwa watu walioko hapo. Tunatoa wito kwa pande zote kusaidia mashirika ya misaada kuwafikia raia na kulinda na kuheshimu shughuli za kibinadamu , wafanyakazi na mali wakati wote. Tumeandaa mpango ambao utatuwezesha kutoa msaada zaidi haraka kwa watu hasa walioathirika saana na mashafuko pamoja na kuendelea kutoa msaada kwa walioondoka Sudan na kwenda kutafuta hifadhi Sudan Kusini kwenye majimbo ya Unity na Nile."