Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

UNMISS yaunga mkono uamuzi wa Muungano wa Afrika kuhusu Sudan Kusini

UNMISS yaunga mkono uamuzi wa Muungano wa Afrika kuhusu Sudan Kusini

Mwakilishi maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa nchini Sudan Kusini, Hilde Johnson ameunga mkono uamuzi wa baraza la amani na usalama la Muungano wa Afrika AU kuhusu kuunda tume ya kuchunguza ukiukwaji wa haki za binadamu nchini humo. Taarifa ya ujumbe wa Umoja wa Mataifa Sudan Kusini, UNMISS imemkariri Bi. Johnson akisema kuwa uamuzi huo umekuja wakati muafaka wakati huu ambapo anatiwa wasiwasi mkubwa kutokana na ongezeko la ukiukwaji wa haki za binadamu. Amesema raia wanauawa na hata askari wanatekwa kwenye sehemu mbalimbali nchini humo akitaja ushahidi kufuatia kugundulika kwa idadi kubwa ya miili huko Juba  na miji ya Malakal na Bor.  Mkuu huyo wa UNMISS ameshutumu vikali ukatili dhidi ya raia wa jamii mbali mbali akisema kuwa hakuna uhalali wowote wa kufanyika vitendo hivyo. Amesema uamuzi wa AU wa kuunda tume ya kuchunguza ukiukwaji wa haki za biandamu na unyanyasaji wa aina nyingine ni kitu cha kuungwa mkono akisema kuwa Umoja wa Mataifa uko kidete na wana Sudan Kusini na unataka pande zote kusitisha ghasia mara moja kwa mujibu wa wito wa nchi wanachama wa IGAD waliokutana Nairobi. Tume hiyo ya AU ikishafanya uchunguzi itatoa mapendekezo ya jinsi ya kuwajibisha wahusika