Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ban alaani shambulio mjini Beirut

Ban alaani shambulio mjini Beirut

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon amelaani vikali shambulio la bomu katika gari mjini Beiruti lililouwa watu sita akiwemo waziri wa zamani wa biashara Muhamed Chatah na kujeruhi kadhaa .

Taarifa iliyotolewa leo mjini New York na msemaji wa katibu mkuu imemnukuu bwana Ban akituma salamu za rambirambi kwa familai za wahanga na kuwatakia uponyaji wa haraka majeruhi. Katibu Mkuu amesema akiwa waziri wa fedha na mshauri wa sera ya mambo ya nje kuwa waziri mkuu marehemu Chatah alitumikia nchi yake bila kuchoka, alikuwa mvumilivu na mfano na hivyo akaongeza kuwa kifo chake ni hasara kubwa kwa Lebanon na sehemu ya funzo la umuhimu wa kukomesha ukwepaji sheria.

Bwana Ban amesema anahuzunishwa na matukio mfululizo ya ugaidi Lebanon amabayo yanahatarisha utulivu na mshikamano wa taifa hilo. Kadhalika amekaribisha juhudi za mamlaka nchini Lebanon na vikosi vya usalama katika kushughulikia changamoto za kiusalama na kulinda nchi dhidi ya madhara ya mzozo wa nchi jirani ya Syria. Katibu mkuu Ban amevitaka vyama vyote nchini Lebanon kuvumilia na kuunga mkono katiba ya nchi hususani vikosi vya usalama katika kuzuia vitendo zaidi vya kigaidi.

Amemaliza ujumbe wake kwa kusisitiza muhimu wa kuwafikisha katika mkono wa sheria watekelezaji wa tukio lililogarimu maisha ya watu akiwamo waziri huyo wa zamani Chatah na kuitaka jumuiya ya kimataifa kuunga mkono usalama na utulivu nchini Lebanon