Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Serikali ya Syria na makundi ya upinzani yathibitisha kushiriki mkutano wa amani

Serikali ya Syria na makundi ya upinzani yathibitisha kushiriki mkutano wa amani

Mwakilishi wa pamoja wa Umoja wa Mataifa na Muungano wa nchi za Kiarabu kuhusu Syria, Lakhdar Brahimi amesema kuwa serikali ya Syria na makundi ya upinzani yamethibitisha kushiriki mkutano wa kimataifa mwezi ujao kuhusu amani nchini Syria, ambao utafaanza Januari 22 mwakani katika mji wa Uswisi wa Montreaux.

Bwana Brahimi amesema, ameambiwa na serikali ya Syria kuwa tayari imewateua wawakilishi wake kwenye mkutano huo, na itawatangaza katika siku chache zijazo.

Amesema makundi ya upinzani bado yanashauriana kuhusu wawakilishi wao kwenye mkutano huo. Ameongeza kuwa zaidi ya nchi 30 wanachama wa Umoja wa Mataifa na mashirika ya kikanda yameelezea kutaka kushiriki mkutano huo.

Hata hivyo, bado kuna sintofahamu kuhusu kushiriki kwa Iran, kufuatia pingamizi kutoka kwa Marekani. Ametoa wito kwa serikali na upinzani kuwaachilia huru watu walokamatwa na kuruhusu misaada ya kibinadamu kuwafikia wanaoihitaji, kama ishara ya uungaji wao mkono harakati za amani.