Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mswada wa ‘NGO’ Sudan Kusini watishia huduma za mashirika ya kiraia: Wataalam wa UM

Mswada wa ‘NGO’ Sudan Kusini watishia huduma za mashirika ya kiraia: Wataalam wa UM

Wataalam watatu maalumu wa Umoja wa Mataifa, leo wameonya kuwa mswada unaojadiliwa sasa na bunge la Sudan Kusini kuhusu mashirika yasiyo ya kiserikali, au NGOs, unatishia kazi na uhuru wa mashirika ya kiraia nchini humo.

Wataalam hao wamesisitiza kuwa kipengee cha uangalizi wa serikali kilichopendekezwa katika mswada huo kinavuka mpaka na kuzidi haja ya kutoa taarifa kwa serikali, na hivyo kuifanya serikali kudhibiti mashirika hayo zaidi ya inavyohitajika kawaida, na kutoa wito kwa serikali kukataa sheria ambayo itaweka vikwazo kuhusu sekta ambazo mashirika ya kiraia yanaweza kujihusisha nazo.

Wameelezea wasiwasi yao kuhusu mwenendo unaotanda sasa wa serikali barani Afrika na kwingineko kuwa na mamlaka zaidi ya kudhibiti mashirika huru kwa kutumia sheria zinazoitwa ‘Sheria za NGO’, na kuongeza kuwa mswada huo wa Sudan Kusini ni ushahidi zaidi wa hali hiyo inayotia hofu kote duniani.

Baadhi ya mambo ulosheheni mswada huo wa ‘NGO’ Sudan Kusini, ni pamoja na mashirika hayo kuhitajika kujiandikisha na kujiandikisha tena, pamoja na kushtakiwa ikiwa hayatatii kikamilifu sheria hiyo ilopendekezwa.