Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Waathirika wa mzozo wa Darfur wamepoteza matumaini: ICC

Waathirika wa mzozo wa Darfur wamepoteza matumaini: ICC

Mwendesha Mashtaka Mkuu wa Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu, ICC, Fatou Bensouda, ameliambia Baraza la Usalama leo kuwa, ingawa Baraza hilo lilipitisha azimio 1593 la kuipeleka kesi dhidi ya Rais Omar al Bashir wa Sudan na wengine kwa mahakama ya ICC na kutoa matumaini kwa waathiriwa wa mgogoro wa Darfur, inahuzunisha kuwa matumaini hayo yamezama.

Bi Bensouda amesema hali Darfur inaendelea kuzoroteka, na hatma ya waathirika kuzidi kuwa mbaya zaidi. Amesema katika kipindi cha miaka kumi, hali ya Darfur imeigharimu Umoja wa Mataifa na mashirika ya kutoa huduma za kibinadamu zaidi ya dola bilioni kumi, na maisha ya wafanyakazi 47 wa kutoa huduma za kibindamu.

Inahuzunisha kuwa, kwa kila ripoti inayotoa ofisi yangu kwa Baraza hili, matumaini ya waathirika wa Darfur yanadidimia. Kwa hii ripoti ya 18, bila shaka matumaini yote yametoweka. Hali Darfur haiendelei tu kutishia usalama wa kimataifa na amani, lakini hali nyingine, kama ya Abyei na ile ya mpaka kati ya Sudan na Sudan Kusini, zimeendelea kuzorota.”

Bi Bensouda pia amesema mashambulizi dhidi ya walinda amani limekua jambo la kawaida, na kwamba kufikia sasa wameuawa walinda amani 57. Amesema huku ofisi yake ikiwaenzi walinda amani walouawa, mashambulizi ya kukusudia yanayowalenga walinda amani wa kimataifa ni uhalifu chini ya sheria ya kimataifa, na kwamba ni wajibu wa jamii ya kimataifa kuhakikisha wanaofanya mashambulizi hayo wanawajibishwa kisheria.