Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ban amteua Shamshad Akhtar wa Pakistan kuwa Mkuu wa ESCAP

Ban amteua Shamshad Akhtar wa Pakistan kuwa Mkuu wa ESCAP

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-Moon, amemteua Bi Shamshad Akhtar wa Pakistan kuwa Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Kiuchumi na Kijamii ya Asia na Pasifiki, ESCAP.

Bi Akhtar atachukuwa mahala pa Bi Noeleen Heyzer wa Singapore, ambaye Ban amemshukuru kwa mchango wake wa kujitoa kwa ESCAP na kwa ukanda wa Asia na Pasifiki kwa ujumla. Bi Heyzer ataendelea kuwa Mshauri Maalum wa Katibu Mkuu kuhusu Timor-Leste, katika kuimarisha ushirikiano uliopo kati ya serikali ya Timor-Leste na Umoja wa Mataifa na juhudi za kujenga amani, kujenga taifa na maendeleo endelevu.

Bi Akhtar, ambaye tangu mwaka 2012 amekuwa Mshauri Mkuu wa Katibu Mkuu kuhusu Maendeleo ya Kiuchumi na Kifedha, na pia Mkuu wa idara ya masuala ya kiuchumi na kijamii, ana uzoefu wa zaidi ya miaka 30 katika utungaji na utekelezaji wa sera za kiuchumi, maendeleo, na kifedha katika nchi yake na kwa ukanda mzima.