Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kifo cha Mandela: Baraza Kuu la UM lasema ni masikitiko makubwa

Kifo cha Mandela: Baraza Kuu la UM lasema ni masikitiko makubwa

Salamu za rambirambi kufuatia kifo cha Mzee Mandela zimeendelea kutolewa na za hivi punde zinatoka kwa Rais wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa John William Ashe ambaye amemwelezea Mzee Mandela kuwa ni alama ya amani duniani na gwiji wa maadili miongoni mwa viongozi wa zama za sasa. Bwana Ashe amesema wakati wa uhai wake alitumia busara zake kuchagua maridhiano badala ya visasi, alitumia matumaini badala ya kukata tama. Rais huyo wa Baraza Kuu amesema wakati huu wa kifo chake ni vyema kila mmoja kuomboleza huku akikumbuka matendo ya Madiba kama alivyojulikana zaidi nchini mwake na miongoni mwa jamii yake. Bwana Ashe amesema kwa Umoja wa Mataifa tarehe 18 Julai ni siku ya Mandela na siku ya leo, Umoja wa Mataifa unaungana na Jumuiya ya kimataifa katika majonzi juu ya kifo chake. Hata hivyo amesema ushujaa wake utaendelea kuwepo kwenye fikra za watu wote duniani.