Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ban alaani vikali shambulizi la bomu Yemen

Ban alaani vikali shambulizi la bomu Yemen

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-Moon, amelaani vikali shambulio la kigaidi lililotekelezwa leo dhidi ya Wizara ya Ulinzi ya Yemen na ambalo limeripotiwa kuwaua watu 20 na kuwajeruhi wengine wengi.

Bwana Ban ametoa wito kwa wote wanaohusika kushirikiana kikamilifu na uchunguzi ulotangazwa kufanyika na Rais Abed Rabbo Mansour Hadi, wenye nia ya kuwawajisbisha waloutekeleza uhalifu huo kisheria.

Amekumbusha kuwa Baraza la Usalama li tayari kuchukua hatua zaidi kukabiliana na vitendo vyovyote vya watu binafsi au makundi ambayo yanalenga kuvuruga harakati za mpito.

Amesema njia pekee ya kufikia taifa la Yemen lenye utulivu, maendeleo na demokrasia ni kupitia katika mazungumzo ya amani yanayoendelea, chini ya makubaliano ya mpito ya maazimio namba 2014(2011) na 2051(2012) ya Baraza la Usalama.