Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Makubaliano ya Bali yaruhusu sera kabambe kuhusu uhakika wa chakula: Mtaalamu UM

Makubaliano ya Bali yaruhusu sera kabambe kuhusu uhakika wa chakula: Mtaalamu UM

Wakati macho na masikio yameelekezwa huko Bali, Indonesia ambako tarehe Tatu mwezi huu kunaanza mkutano wa siku tatu wa mawaziri wa nchi wanachama wa shirika la biashara duniani, WTO,  wito umetolewa kwa nchi zinazoendelea kupatiwa uhuru wa kutumia chakula cha akiba kwa ajili ya hakikisho la usalama wa chakula bila ya woga ya vitisho vya kuwekewa vikwazo kwa mujibu wa kanuni za sasa za shirika hilo.

Mtaalamu maalum wa Umoja wa Mataifa kuhusu uhakika wa chakula Olivier De Schutter amesema hayo wakati ambapo washiriki wa mkutano huo watajaribu kufikia makubaliano juu ya mapendekezo ya chakula cha akiba kwa nchi zinazoendelea kwa minajili ya uhakika wa chakula kama sehemu ya mashauriano ya Doha.

De Schutter amesema kanuni za biashara zinapaswa kuandaliwa kwa kuzingatia sera za uhakika wa chakula ambazo nchi zinazoendelea zinahitaji badala ya kuwa na sera ambazo zinatoa kipaumbele kwa kanuni za WTO. Amesema kusaidia uzalishaji chakula kwenye nchi zinazoendelea ni msingi muhimu wa kwanza katika kufikia lengo la haki ya chakula badala ya kupatia kipaumbele biashara.

Mtaalamu huyo ameonya kuwa uhakika wa chakula uko hatarini zaidi kwa nchi hizo ambazo zinaendelea kutegemea zaidi masoko ya duniakamailivyodhihirika kwenye mzozo wa chakula duniani mwaka 2007-2008.

De Schutter amesema ni lazima mkutano huo uandae sera kabambe na bunifu kuhusu uhakika wa chakula ambazo zitatoa usaidizi kwa sekta ya uzalishaji  ya nchi husika kwa kuzingatia uzoefu wa nchi nyingine kadhaa zilizofanikiwa kwa kufanya hivyo.