Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Utumwa ni ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu: Ashe

Utumwa ni ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu: Ashe

Ikiwa leo ni Siku ya Kimataifa ya kutokomeza utumwa, rais wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa, John William Ashe, amesema utumwa wa nyakati za sasa ni ukiukwaji mkubwa wa haki za kimsingi za binadamu. Joshua Mmali na taarifa kamili.

(TAARIFA YA JOSHUA)

Katika ujumbe wake kuadhimisha siku hii, Bwana Ashe amesema utumwa huenda umekuwa, na unaendelea kuwa janga kubwa zaidi katika historia ya mwanadamu.

Ameongeza kuwa, hata unapotokomezwa, utumwa unaacha makovu ya daima kihisia, na unaweza kuvuruga familia na kuwafanya watu wasiwe na uwezo wa kurejelea tena jamii zao.

Ametoa wito kwa nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa kutokomeza aina zote za utumwa, na kuchagza mikakati inayoendeleza ujumuishaji wa kijamii na kutokomeza aina zote za ubaguzi.

Naye Katibu Mkuu Ban Ki-Moon ametoa wito wa kuungana katika juhudi za kuwa ulimwengu usio na utumwa. Katika taatifa yake kuadhimisha siku hii, Ban amesema utumwa wa wakati huu huwaathiri watu walio fukara zaidi, hususan makundi yalotengwa kijamii, wakiwemo wahamiaji, wanawake, kabila zilizotengwa na watu wa asili.